August 30, 2016




WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema wafanyabiashara wanaokwepa kulipa kodi wanaiathiri Serikali katika juhudi zake za kuboresha maisha ya Watanzania.

Amesema Serikali haina mgogoro na wafanyabiashara bali inawataka walipe kodi na kama kuna wanaonewa na watendaji wa chini kwa kubambikiziwa kodi watoe taarifa juu ya jambo hilo.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, 30 Agost, 2016) wakati akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Makampuni ya Mohamed Enterprises Tanzania Limited (MeTL), Mohamed Dewji, ofisini kwake jijini Dar es Salaam.

Amesema Serikali imedhamiria kuwaunga mkono wafanyabiashara katika shughuli zao ili waweze kulipa kodi itakayoifanya imudu kuwahudumia wananchi katika huduma mbalimbali za jamii.

“Sisi msisitizo wetu ni ulipaji kodi, wakwepa kodi wanatuathiri. Sekta nyingine zinashindwa kuendelea kwa sababu hazina mtaji na kodi hazipatikani vizuri,” amesema.

Amesema “Ninyi timizeni wajibu wenu kwa kulipa kodi stahiki, tutawasaidia katika kufanya biashara zenu. Tutawasaidia katika kusimamia mambo yenu ila mjue kwamba nchi hii bila viwanda hatuwezi kwenda,”.

Pia amewataka wafanyabiashara kwenda kujenga viwanda katika maeneo ambayo malighafi zinazalishwa ili kuwahamasisha wakulima kuzalisha zaidi na kuwapunguzia mzigo wa kusafirisha malighali hizo.

Kwa upande wake Dewji amemuhakikishia Waziri Mkuu kwamba wafanyabiashara wanaiunga mkono Serikali ya Awamu ya Tano na hawana mpango wowote wa kuhamishia mitaji yao nje ya nchi kama inavyodaiwa na baadhi ya watu.

“Huu ni uongo na uzushi tu ambao watu wameamua kuusambaza, mfano mimi mwenyewe nimeanza kuongeza mitaji katika biashara zangu. Nimefufua kiwanda cha kuchambua pamba cha Chato. Nafungua biashara zingine mpya kubwa ikiwemo ya kufufua kiwanda cha nguo cha Musoma ambacho kitakuwa kinatengeneza jeans za kuuza nje ya nchi,” amesema.

Amesema yuko tayari kuwekeza kwenye ujenzi wa kiwanda cha sukari katika wilaya ya Rufiji mkoani Pwani. Kiwanda hicho kitakuwa na uwezo wa kununua miwa tani milioni 1.2 zitakazozalisha tani 120,000 za sukari kwa mwaka.

Mkurugenzi huyo amesema amepanga kuwekeza sh. bilioni 40 kwa ajili ya kukuza uzalishaji katika mashamba yake ya mkonge kwenye mikoa ya Pwani, Tanga na Morogoro.

Pia amewekeza sh. bilioni 70 katika viwanda vya kusaga unga wa ngano na sembe na anatarajia kununua tani laki moja za mahindi katika msimu wa mwaka huu.

Mbali na kuwekeza katika viwanda hivyo Dewji amesema anatarajia kujenga kiwanda kikubwa cha kutengeneza sabuni ya unga ambacho kitakuwa ni kikubwa kuliko vyote katika nchi za Afrika Mashariki na Kati.

“Tumeamua kuongeza uwekezaji katika viwanda ili kuunga mkono mkakati wa Serikali wa kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda. Vile vile nimefanikiwa kuishawishi kampuni kubwa na maarufu ya kutengeneza sigara duniani ya Marlboro kuingia nayo ubia na sasa tunajenga kiwanda cha sigara hizo mjini Mrogoro,” amesema.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S. L. P. 3021,
11410 DAR ES SALAAM.
JUMANNE, AGOSTI 30, 2016.

0 MAONI YAKO:

Post a Comment

Popular Posts

WADAU

BLOG ZINGINE