Wiki moja baada ya kuwa gumzo kuu katika mkutano mkuu wa
Chama Cha Mapinduzi (CCM), Edward Lowassa, Waziri Mkuu Mstaafu ambaye
aligombea urais katika uchaguzi mkuu mwaka jana, Jumapili 30 Novemba
2016 saa 3.00 asubuhi atafunguka juu ya mengi yanayosemwa juu yake.
Lowassa ambaye ni mjumbe wa Kamati kuu ya Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (Chadema) atazungumza kupitia kipindi cha “Funguka”
kinachoendeshwa na mwandishi wa habari nguli Tido Mhando kupitia kituo
cha televisheni cha Azam 2.
Katika taarifa iliyotolewa leo na Azam 2 inasema “Lowassa atafafanua na kueleza mengi kuhusu maisha yake marefu kisiasa”.
Aidha, Lowassa ambaye aligombea urais kwa tiketi ya Chadema, huku
akiungwa mkono na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa)
amekuwa kimya kwa muda mrefu licha ya kuzungumzwa, kuandikwa kuelezwa na
kutendewa mengi yanayomhusu bila yeye binafsi kujitokeza hadharani na
kujibu.
Gumzo la Lowassa ndani ya mkutano mkuu wa CCM lililoenda sambamba na
baadhi ya viongozi na wazungumzaji kumshambulia wazi wazi huku
wakishidwa kujadili kwa kina mambo yanayohusu chama, linatajwa kuwa ni
hofu ya CCM dhidi ya Lowassa.
Hayo yatajiri ikiwa ni siku tatu tangu aadhimishe mwaka mmoja tangu
kuhama CCM na kuwataka wanaomuunga mkono wakiwa CCM waendelee kumpa siri
za mambo yanayojiri CCM ikiwemo mikakati ya Rais Magufuli.
CHANZO: MWANAHALISI
BY: EMMY MWAIPOPO
0 MAONI YAKO:
Post a Comment