April 28, 2024


Mbunge wa Jimbo la Morogoro Mjini Mhe, Dkt. Abdulaziz M. Abood ameutaka uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro kugawa vizimba katika Soko la Machinga Complex lililopo maeneo ya FIRE  kwa watu na wafanyabiashara waliokusudiwa na ambao wanahitaji vizimba hivyo ili kukuza na kuboresha mitaji ya wafanyabiashara wadogo.

Mhe Abood ametoa kauli hiyo katika shughuli za uwekaji wa jiwe la Msingi kwenye Soko hilo Aprili 27 Mwaka huu mbele ya kiongozi wa mbio za Mwenge wa uhuru ndugu Godfrey Mzava, wakati Mwenge, ulipotembelea Mradi huo kwa ajili ya kuukagua na kujionea maendeleo ya Mradi hadi uliopofikia.

Mhe Abood ameweka wazi kuwa, Mradi huo umegharimu kiasi cha shilingi Mil. 696, fedha ambazo zimetokana na mapato ya ndani ni kiasi cha Shilingi Mil. 199 na kiasi cha shilingi Mil. 497 zimetolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kujenga Soko hilo ili kuondoa kero kubwa iliyokuwa inawakabili wafanyabiashara wadogo wadogo waliokuwa wakiuza bidhaa zao kwa kutangatanga mitaani na kando kando ya barabara na sasa wawe na eneo maalum na lenye uhuru kwa ajili ya kuendesha biashara hizo.

Aidha, Mhe Abood amekemea tabia za baadhi ya watumishi ambao inapofika wakati wa kugawa vizimba kwa ajili ya wafanyabiashara hao, huchukua wao kisha kuwapangisha wenye mahitaji stahiki, jambo ambalo linaongeza chuki baina ya wananchi na Serikali yao, hivyo ili kuepukana na hilo Mhe Abood ametaka Vizimba hivyo kugawiwa kwa  waliolengwa na waweze kufanyabiashara ili kujikimu Maisha yao na familia zao.

“Wakati unapofika wa kugawa vizimba vya Soko hili, nashauri tuzingatie walengwa kwanza kwa sababu hadi kujengwa kwa Soko hili wao ndio kipaumbele, kwani wao ndo wanaoteseka na kutangatanga barabarani hadi Mhe Rais amewaona na kuamua kutoa fedha ili kujenga Soko hili. Tusije tukawapa watu wasiostahili halafu wakawapangisha wahitaji” Amesema Mhe Abood.

Kwa upande wake kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru amekagua Jengo la Soko hilo na kuridhishwa na maendeleo ya mradi huo, hivyo kuamua kuliwekea jiwe la Msingi la ujenzi wa Soko hilo, amesisitiza kuwa miradi yote ya kimaendeleo ambayo Rais Samia anatoa fedha ili kukamilisha miradi, lazima miradi hiyo isimamiwe kikamilifu kama ambavyo mradi huu umesimamiwa vema.
Katika hatua nyingine, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru ametembelea Kituo cha watoto wenye mahitaji maalum cha Mihayo kilichopo Kata ya Mazimbu ambapo Mwenge huo umetoa zawadi ya matihaji ya kibinadamu kama Mchele kg 250, Unga wa Sembe kg 100, Sukali kg 75, Unga wa Ngano kg 50, Maharagwe kg 50, Mafuta ya kupikia lita 60, Sabuni ya mche katoni 1, Chumvi katoni 1, Mbuzi 1, Sabuni ya unga kg 15, Tisheti pamoja na Mashuka 13.

Naye Mhe Rebeka Msemwa Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, amemuhakikishia Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru ndugu Godfrey Mzava kuwa, wananchi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro wanamshuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwaletea fedha zaidi ya Bil. 3 ambazo zimeweza kuzalisha miradi ya kimaendeleo ambayo imepitiwa na kukaguliwa na Mwnge wa Uhuru katika Manispaa hiyo.

Sanjari na hayo, Mwenge wa Uhuru umefanikiwa kuzindua Shule mbili zilizojengwa wa Mradi wa Boost kutoka Serikali Kuu, Shule moja ya Msingi iitwayo Viwandani  iliyopo Kata ya Mafisa ambayo watoto wameshaanza kusoma na ujenzi wake umekamilika kwa 100%, na ya pili ni Shule ya Sekondari ya Mkundi Mlimani ambayo nayo pia imezinduliwa leo kupitia Mbio za Mwenge huo.

Imetolewa na: Kitengo cha Habari na Mawasiliano Ofisi ya Mbunge

0 MAONI YAKO:

Post a Comment

Popular Posts

WADAU

BLOG ZINGINE