Leo ni tarehe 8 Machi katika kalenda ya Kimataifa, imepewa jina la "Siku ya Wanawake."
Ukweli ni kuwa siku hii ni siku kwa ajili ya kukumbusha hali waliyonayo wanawake duniani, pamoja na matatizo na masaibu yanayowakabili. Katika dunia ya leo licha ya kauli nyingi za kilaghai na za kupumbaza nyoyo, wanawake wengi katika maeneo mbalimbali duniani si tu kuwa wanashindwa kupata haki zao za kimsingi, bali pia wanaishi katika mazingira magumu sana.
Katika nchi nyingi duniani, wanawake na watoto huwa wahanga wa kwanza wa vita na mapigano. Katika nchi za Kiafrika pia kama Sudan Kusini, Nigeria, Burundi na Jamhuri ya Afrika ya Kati, wanawake ni waathirika wakuu wa masuala hayo yaliyotajwa. Huko Sudan Kusini wanawake wengi wanauliwa au kukamatwa mateka, huku wakikabiliwa na udhalilishaji wa kingono kama kubakwa na kufanywa watumwa wa ngono.
Huko Jamhuri ya Afrika ya Kati pia wanawake na watoto wanakabiliwa na hali hiyo hiyo. Hata wanawake wengi ambao wanaishi katika kambi za Umoja wa Mataifa hawapati haki zao za msingi. Hii ni katika hali ambayo sualal la udhalilishaji wa kingono unaofanywa na wanajeshi wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa, vikosi ambavyo vilipasa kuwadhaminia wanawake usalama wao, ni changamoto nyingine katika kukosekana uthabiti na kuweko vitendo vya udhalilishaji wa kingono dhidi ya wanawake.
Mbali na wanawake wanaoishi katika nchi zenye vita na machafuko, hata wale walioko kwenye nchi zenye amani ya wastani nao pia hawapati fursa ya kwenda mashuleni na hivyo kukosa haki ya kujipatia elimu. Masuala kama njaa na lishe dunia pia yanatishia maeneo mengi ya Afrika, ambayo idadi kubwa ya watu wake ni wanawake na watoto.
Harakati na hujuma za makundi ya kigaidi yenye misimamo ya kufurutu ada katika aghalabu ya nchi za Kiafrika ni jambo jingine linalowatumbukiza wanawake katika hali ya hatari ya kufikwa na madhara kubwa. Magaidi wengi huwateka nyara wanawake na watoto katika mashambulizi yao ya kigaidi na kisha huwatumia kwenye oparesheni zao za kijeshi na za kujilipua na mabomu. Ni zaidi ya mwaka mmoja hadi sasa ambapo hakuna taarifa yoyote wala kujuklikana hatima ya wasichana 241 wa shule moja ya sekondari nchini Nigeria waliotekwa nyara wakiwa shuleni.
Soyota Maiga, Naibu Mkuu wa Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu na Mataifa amesema kuwa wanawake na watoto ni wahanga wakuu wa mizozo ya ndani inayojiri katika nchi mbalimbali za Afrika na kwamba wanawake wanakabiliwa na ukatili na udhalilishaji wa kingono; ambapo wahusika wa vitendo hivyo husalia hivi hivi bila ya kupewa adhabu yoyote.
Lakini mbali na Afrika, katika maeneo mengine ya dunia pia wanawake wanakabiliwa na hali ngumu na wanaishi bila ya amani. Wanawake wengi waliopata hifadhi katika mipaka ya nchi za Ulaya wanaishi katika mazingira magumu; na wale ambao wameweza kuvuka mipaka na kupewa hifadhi makambini, hawapati misaada wala usalama wa kutosha.
Shirika la Msamaha Duniani (Amnesty International) limetangaza katika ripoti yake mpya kuwa wanawake wahajiri ambao baadhi yao wanatoka katika nchi za Kiafrika, daima hukabiliwa na vitisho vya kubakwa na kudhalilishwa kijinsia katika awamu zote za safari zao kuelekea Ulaya.
Ripoti ya Amnesty International imesisitiza kuwa, wanawake wote wanaohajiri katika nchi za Ulaya wamekuwa wakihisi hatari na kukosa amani wakiwa safarini huku wakitendewa miamala ya utumiaji mabavu, kubakwa na kufanywa watumwa wa ngono na wahusika wa magendo ya binadamu na vikosi vya usalama. Aidha katika nchi nyingine nyingi wanawake wanashindwa kupata haki yao ya msingi ya kuishi katika mazingira ya amani sambamba na kustafidi na suhula bora za kimaisha, kupata haki ya elimu n.k. Wanawake wengi ambao wametekwa nyara katika nchi hizo na kundi la kigaidi la Daesh, hukabiliwa na vitendo vibaya zaidi vya utumiaji mabavu. Huko Iraq aghalabu ya wanawake wa Kiizadi waliotekwa nyara na Daesh, wameuzwa katika soko la kuuzia watumwa huku hatima ya wanawake wengine wa kabila hilo ikiwa haijulikani.
Uhuru, usawa, kulinda haki, kuwa na amani na usalama, ni miongoni mwa shaari na kaulimbiu nzuri na zenye kutia moyo ambazo zinanadiwa kila siku na viongozi wengi wa nchi za Magharibi kwa maslahi yao; huku nchi hizo zikishuhudiwa kushiriki nyuma ya pazia katika vita na mizozo mingi inayojiri katika nchi nyengine kwa kuzipatia misaada ya kijeshi na silaha pande zinazozozana katika nchi hizo
0 MAONI YAKO:
Post a Comment