November 21, 2016

mkuu-wa-mko-wa-dar-es-salaam-paul-makonda-akizungumzana-watumishi-wa-wilaya-temeke 

 Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amesema ataanza kuwastaafisha watumishi wa umma wasiowajibika huku akidai katika ofisi yake ni wakuu wa idara wanne pekee ndio wanaofanya kazi vizuri kati ya watumishi 120.
Aidha amesema kuwa daima haogopi kutumbuliwa jipu kama wengi wanavyo muombea na kwamba yuko tayari kugombana na mtu yoyote kwa kutetea wananchi.
Alisema tayari amewasiliana na ngazi za juu za serikali, ili kuona uwezekano wa kuwapunguza watumishi hao ikiwa ni pamoja na kuwastaafisha kwa manufaa ya umma.
“Watu hawawajibiki. Wanakula tu mishahara ambapo katika bajeti yetu ya sh.bilioni 600 ni bilioni 100 tu ambazo zinaelekezwa kwenye sekta ya maendeleo. Sh.bilioni 400 zinaishia kuwalipa mishahara na mambo mengine, huku wananchi wakiendelea kuteseka na changamoto,”alisema Makonda.
Alisema kuna watendaji ambao hawana ubunifu na wengi wamekuwa wakijitetea kuwa hawana bajeti au hawajapata bajeti hizo bila kubuni njia za kutatua changamoto za wananchi.
“Hatuwezi kwenda kwa namna hii. Tutawajibishana tu na tutatumia njia za kuwawajibisha ikiwemo ya kuwastaafisha kwa manufaa ya umma,”alisema Makonda.
Aliongeza “Mimi siogopi kutumbuliwa jipu na niko tayari kukosana na kila mtu huku nikitetea wananchi wangu. Siwezi kuvumilia kuona wakuu wa idara na watumishi wa umma wakikaa ofisini bila kuwajibika,”
Akizungumza na watumishi wa halmshauri hiyo, madiwani, wenyeviti wa serikali za mitaa na wabunge wilayani Temeke, leo, Makonda alisema, hayuko tayari kumvumilia mtendaji yoyote ambaye hawajibiki ipasavyo katika kutatua kero za wananchi.
“Ninataka uwajibikaji, kuanzia serikali ya mtaa hadi idara. Kila mtu awajibike kwa nafasi yake. Atakayeshindwa ajiondoe la sivyo tutamstaafisha au kumpunguza. Watendaji wasiyo wajibika wajihesabie kuwa wanabahati mbaya ya kuwa viongozi katika mkoa huu,”alisema Makonda.
Akiwasilisha ripoti ya wilaya, Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Felix Lyaniva, alisema wamejipanga kikamilifu hususan katika kukabiliana na kero za wananchi, kusimamia ukusanyaji wa mapato, kumaliza changamoto ya madawati ambapo hivi sasa wana wanashughulikia changamoto ya vyumba vya madarasa na uhalifu.

0 MAONI YAKO:

Post a Comment

Popular Posts

WADAU

BLOG ZINGINE