Imepita miaka 15 tangu kujiri mashambulizi ya
kigaidi ya Septemba 11 nchini Marekani. Miaka 15 iliyopita tarehe 11
Septemba 2001, Marekani ilikumbwa na mashambulizi ya kigaidi
yaliyoutikisa pia ulimwengu.
Kitovu cha kijeshi na uchumi cha taifa hilo vililengwa na
hujuma za kundi la kigaidi la al-Qaaidah. Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa
ardhi ya nchi hiyo kushuhudia hujuma za adui wa nje baada ya kupita
miaka 189. Aina ya shambulio hilo, nyenzo zilizotumika kufanyia
shambulio lenyewe, maeneo yaliyolengwa na ukubwa wa maafa ya roho za
watu na hasara ya mali iliyosababishwa na hujuma za Septemba 11
zilibadilisha siasa, uchumi na utamaduni wa Marekani; kiasi kwamba,
tunaweza kuyagawa matukio na hali ya Marekani katika vipindi viwili, cha
kabla na baada ya Septemba 11.
Ndege za kijeshi za Marekani zikidondosha mabomu nchini Afghanistan mwaka 2001
Hata hivyo isisahaulike kwamba hadi sasa kuna dhana nyingi kuhusiana
na tukio hilo huku baadhi ya maswali yakiwa bado hayajapatiwa majibu.
Pamoja na kutafakari kuhusu nini kilijiri asubuhi ya tarehe 11 Septemba
na watu gani waliohusika katika operesheni hizo, athari za tukio hilo
ndizo ambazo zimekuwa na umuhimu zaidi kwa jamii ya walimwengu. Baada ya
tukio la Septemba 11, 2001 ulimwengu uliingia kwenye kipindi
kisichokuwa na mlingano katika vita, mauaji na machafuko. Katika
radiamali yake serikali ya wakati huo ya Marekani iliingia katika vita
vya kile ilichodai kuwa ni kupambana na 'ugaidi' na moja kwa moja
ikazishambulia nchi mbili za Afghanistan na Iraq. Sambamba na uingiliaji
huo kulianza pia operesheni za kijeshi kwa lengo la kukabiliana na
mtandao wa ugaidi duniani. Wakati huo, madola ya Magharibi yakiongozwa
na Marekani yakakanyaga wazi wazi mipaka iliyoainishwa katika kuchunga
faragha ya mtu binafsi na kadhalika sheria za haki za binaadamu na
sheria za kivita katika vita vyao hivyo dhidi ya ugaidi.
Askari wa Marekani wakianza kuingia ardhi ya Afghanistan ili kuikalia
Pamoja na hali hiyo na licha ya miaka 15 kupita baada ya tukio la
Septemba 11, ndio kwanza wimbi la ugaidi na makundi ya kufurutu mpaka
kwa ngazi tofauti vimeshadidi zaidi ya kipindi cha kabla ya hujuma hiyo.
Hadi sasa makundi ya kigaidi na kitakfiri kama vile Daesh (ISIS) na
Boko Haram yanatekeleza hujuma zao katika maeneo tofauti ya dunia,
ambapo hujuma zao hizo haziwezi hata kulinganishwa na zile za kundi la
al-Qaidah. Katika kipindi hicho cha miaka 15, nusu ya eneo zima la
Mashariki ya Kati hivi sasa inashuhudia mapigano na vita vya kubuniwa
kwa lengo la kuziweka katika eneo hilo tawala vibaraka za madola hayo ya
Magharibi. Mbali na hayo kiasi cha fedha ambacho kimetumiwa na Marekani
na Ulaya katika kipindi hicho, kimepelekea kuibuka mgogoro mkubwa wa
kiuchumi kwa madola hayo hayo ya Magharibi, mgogoro ambao umeyaweka
maisha ya mamilioni ya watu duniani katika mashinikizo makubwa. Mbali na
hayo kiwango cha Wamagharibi hao katika kusimamia haki za binaadamu,
kimezidi kudhoofika siku hadi siku.
Askari wa Marekani pia wakilinda zao la mpopi kwa ajili ya kujitajirisha
Kupitia vita hivyo dhidi ya ugaidi ndipo kukaibuka jela zenye majina
ya kutisha kama vile Abu Ghuraib na Guantanamo na kupelekea kuliweka
jina la Marekani katika orodha ya nchi zinazoongoza kwa utesaji na
unyanyasaji mkubwa wa wafungwa. Wakati huo huo na kwa kisingizio cha
kukabiliana na ugaidi, ulimwengu ukashuhudia pia ongezeko kubwa la
operesheni za ujasusi ambazo hazikuwahi kushuhudiwa katika historia ya
mwanadamu zinazofanywa na Marekani kiasi kwamba hata viongozi waitifaki
wa Washington nao waliandamwa na ujasusi huo. Kwa hakika tukio la
Septemba 11 mwaka 2001, liliathiri uwiano baina ya uhuru na usalama,
kiasi kwamba ni baada ya hapo ndipo madola hayo yakapiga teke uhuru na
usalama kote duniani. Hadi sasa ni maeneo machache sana ambayo
hayakabiliwi na hatari ya mashambulizi ya kigaidi, suala ambalo
linaashiria kuhusika kwa Marekani katika kuasisi saratani ya ugaidi
baada ya tukio la Septemba 11. Kwa msingi huo, tunaweza kusema kuwa,
kile kinachotajwa kama matunda na mafanikio ya vita dhidi ya ugaidi
baada ya shambulio la Septemba, ni matokeo yasiyo na tija wala faida
yoyote kwa ulimwengu.
0 MAONI YAKO:
Post a Comment