August 12, 2017

  Image result for Wallace Karia 
 
Na Mwandishi Wetu, DODOMA
WALLACE KARIA ndiye Rais mpya wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), baada ya kuibuka kidedea katika uchaguzi uliofanyika leo kwenye ukumbi wa mikutano wa jengo la St. Gasper mjini Dodoma.
Karia amewashinda mchezaji wa zamani wa timu ya taifa, Ally Mayay, Katibu wa zamani wa shirikisho hilo, Frederick Mwakalebela, Mwenyekiti wa zamani wa klabu ya Yanga, Wakili Imani Madega, Mwandishi wa Habari za Michezo wa zamani, Shija Richard na Katibu wa klabu ya Mbeya City, Emmanuel Kimbe.
Michael Richard Wambura ameshinda nafasi ya Umakamu wa Rais akiwaangusha Mwenyekiti wa FA ya Dodoma, Mulamu Nghambi, mchezaji wa zamani wa timu ya taifa, Mtemi Ramadhani, Robert Selasela na Stephen Mwakibolwa. Baada ya matokeo hayo, washindi wote wa waliapishwa kwa agizo la Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe
Ikumbukwe aliyekuwa Rais wa TFF, Jamal Malinzi ameshindwa kurudi kutetea nafasi yake baada ya kuweka rumande tangu Juni 29, mwaka huu kwa pamoja na Katibu weke, Selestine Mwesigwa na Isinde Isawafo Mwanga kwa tuhuma za ubadhirifu.
Watatu hao walipelekwa rumande Juni 29 baada ya kusomewa mashitaka 28 ya kughushi na kutakatisha fedha kupitia akaunti ya TFF iliyopo katika banki ya Stanbic, Dar es Salaam.
Katika mashitaka hayo, 25 yanakwenda moja kwa moja kwa Rais wa shirikisho hilo, Malinzi akidaiwa kughushi michakato mbalimbali ya kifedha, huku matatu yakiwahusu wote na Katibu wake na Mhasibu wake Nsiande Isawafo Mwanga.
Malinzi aliingia madarakani TFF Oktoba mwaka 2013 baada ya kupata kura 72 kati ya 126 zilizopigwa akimshinda aliyekuwa mpinzani wake wa karibu, Athumani Nyamlani, lakini baada ya kesi hiyo kuanza kuunguurma na kuwekwa rumande, Kamati ya Utendaji ya TFF ilikutana na kumteua Makamu wake, Wallace Karia kukaimu Urais wa shirikisho hilo.

0 MAONI YAKO:

Post a Comment

Popular Posts

WADAU

BLOG ZINGINE