April 08, 2014

Mwanafunzi Witness Mbalinga alipokuwa akiongea na wanahabari juzi nyumbani kwao Mtwivilla


Hapa ndipo mwanafunzi huyo anapoishi
 “KAANDIKENI mnachoweza kuandika, ila mimi mtoto wangu hasomi shule ya kata ni bora akae nyumbani mpaka nitakapopata ada ya kumlipia katika shule ya bweni,” haya ni majibu ya mama mzazi wa Witness Mbalinga (13), Menciana Mbalinga aliyeyatoa kwa wanahabari juzi.
Wanahabari hao akiwemo mwandishi wa mtandao huu walikuwa wakifuatilia sakata la mama huyo kumzuia binti yake huyo kujiunga katika shule ya sekondari ya Mtwivilla baada ya kufaulu mtihani wa darasa la saba.
Tangu wanafunzi wenzake wajiunge na elimu hiyo Januari mwaka huu, Witness aliyemaliza shule ya msingi Mtwivilla mwaka jana na baadae kuchaguliwa kujiunga na shule ya sekondari ya Mtwivilla anashinda nyumbani kama binti wa kazi.
Huku akitokwa na machozi binti huyo aliwaeleza waandishi wa habari waliofanikiwa kufika nyumbani kwao mtaa wa Mtwivilla, mjini Iringa kwa mahojiano naye kwamba; “nina miezi mitatu sasa niko tu nyumbani, mama hataki nisome shule ya kutwa.”
Alisema baada ya kukataliwa kujiunga katika shule hiyo ya sekondari ya Mtwivilla, mama yake huyo alimpeleka wilayani Kilolo ambako alifanya mtihani wa kujiunga na shule ya sekondari ya St Michael.
“Nilifanya mtihani na nikafaulu lakini siku zinazidi kwenda na kila nikijaribu kuuliza mama amekuwa akinizungusha,” alisema.
Witness alisema hatma yake ya elimu iko mikononi mwa mama yake huyo aliyemuahidi kumpeleka katika shule hiyo ya bweni leo Jumapili.
Pamoja na kutokwa machozi, Witness aliongea kwa kujiamini huku akionesha kiu aliyonayo ya kuendelea na masomo ya sekondari hata katika shule aliyochaguliwa kujiunga nayo.
Wakati akizuiwa kuendelea na masomo ya sekondari, mzazi huyo ametuhumiwa kumzuia bintiye kwenda kwa ndugu zake kwa kile kilichoelezwa na binti huyo kwamba hataki suala hilo la hatma yake ya shule lilete mjadala ndani ya familia.
“Nina amini kama marehemu baba yangu angekuwa hai, ningekuwa shule kama ilivyo kwa wanafunzi wenzangu,” alisema na kuongeza kwamba baba yake mzazi alifariki miaka minne iliyopita.
Katika majibu yake kuhusiana na tuhuma hiyo mama mzazi wa binti huyo alisema “kilichonikwamisha ni fedha ya kodi ninayopata kutoka katika meza ya biashara aliyokuwa akifanyia mume wangu katika soko kuu la mjini Iringa.”
“Pamoja na kutolipwa, nawahakikishia jumapili hii lazima nimpeleke shule kwasababu kuna mtu ameahidi kunikopesha,” mama huyo anayeendesha mgahawa katika jengo la IMUCU mjini Iringa alisema.
“Mie sina kosa kwasababu sina mpango wa kuona mtoto wangu anabaki nyumbani, yule ni mtoto wangu na ni lazima atapata haki yake ya elimu kama watoto wangu wengine,”alisema.
Bila kuwataja majina alisema anao shemeji na wifi zake wengi mjini Iringa ambao mbali na kutofika nyumbani kwake kujua hali ya familia yake baaada ya mumewe kufariki, hawana msaada wowote kwake na watoto wake.
Alipoulizwa kwanini kama hakuwa na maandalizi ya kutosha ya kumpeleka binti yake shule ya bweni hakumuacha aendelee na masomo katika shule hiyo aliyochaguliwa mpaka pale ataakapokamilisha maandalizi yake?: alisema;
Nia yake nzuri ya kumpeleka mwanae huyo katika shule ya bweni ilikwamishwa na wadeni wake waliochelewa kumpa fedha zake kwa wakati kama walivyokuwa wamekubaliana.
Mapema mwaka huu, Meya wa Manispaa ya Iringa Amani Mwamwindi alitoa agizo kwa madiwani wote wa halmashauri hiyo kuwasaka wanafunzi ambao hawajulikani waliko baada ya kuchaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari.
“Hatuwezi kukaa kimya, tunataka vijana wetu wapate elimu; ni lazima tujue vijana hao wako wapi kwasababu tulikuwa nao katika kata zetu wakiwa katika shule za msingi,” alisema

Source:seetheafrica.blogspot.com/

Related Posts:

0 MAONI YAKO:

Post a Comment

Popular Posts

WADAU

BLOG ZINGINE