Taarifa iliyotolewa na Jukwaa hilo jana na
kusainiwa na mwenyekiti wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Askofu Dk
Alex Malasusa, mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki
Tanzania (TEC), Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa na mwenyekiti wa Kanisa
la Pentekoste Tanzania (CPCT), Askofu Daniel Awet, imetaja sababu mbili
za uamuzi wake kuwa ni muswada wa Mahakama ya Kadhi kukiuka misingi ya
Taifa kuwa na Serikali isiyo na dini, na Kura ya Maoni kusababisha
mgawanyiko.
“Hivyo basi, Jukwaa linawataka waumini wake wote
wajitokeze kwa wingi kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga
Kura, waisome Katiba Inayopendekezwa na kushiriki kikamilifu vipindi vya
elimu juu ya Katiba Inayopendekezwa na kisha wajitokeze kwa wingi
kupiga kura ya hapana kwa Katiba Inayopendekezwa kwa sababu zilizotajwa
hapo juu,” linasema tamko hilo la kurasa nne.
Taarifa hiyo imekuja siku moja tu baada ya Waziri
Mkuu Mizengo Pinda kutangaza kuwa muswada wa uanzishwaji wa Mahakama ya
Kadhi uliokuwa umeondolewa kwenye mkutano uliopita wa Bunge kwa ajili ya
mashauriano zaidi, utawasilishwa katika vikao vya chombo hicho
vinavyoanza Jumanne ijayo baada ya kufikiwa kwa maridhiano baina ya
viongozi mbalimbali wa dini.
Pia tamko hilo limekuja siku chache baada ya Rais
Jakaya Kikwete kuiagiza Hazina itoe fedha kwa Tume ya Uchaguzi (Nec) kwa
kadri inavyohitaji ili kuiwezesha kukamilisha mchakato wa Kura ya
Maoni.
Viongozi wa Jukwaa la Wakristo walikutana Machi
10, mwaka huu kujadili kwa kina kuhusu hali ya usalama wa nchi ilivyo
sasa na mustakabali wake, Katiba inayopendekezwa na uanzishaji wa
Mahakama ya Kadhi.
Katiba inayopendekezwa
Taarifa hiyo ya maneno 712 inasema: “Katiba
Inayopendekezwa imeleta mgawanyiko mkubwa katika Taifa kwani imepatikana
kwa njia zisizo za kiadilifu na mchakato wake umeendeshwa kwa hila na
ubabe.
“Pia haijajibu matakwa na malalamiko ya wananchi
kwenye masuala mbalimbali kama muundo wa Serikali, miiko na maadili ya
viongozi wa umma, haki za binadamu, madaraka ya rais na uwiano wa
mihimili ya dola.
“Ikumbukwe Katiba Inayopendekezwa ilipitishwa
kwenye Bunge Maalumu la Katiba kwa ahadi ya Serikali kuipa dini ya
Kiislam Mahakama ya Kadhi. Inashangaza kuwa hata Serikali inatoa rushwa
ili kufikia malengo yake. Kwa hali kama hii, Kanisa haliwezi kuunga
mkono kupitishwa kwa Katiba Inayopendekezwa,” ilisema sehemu ya tamko
hilo.
Mahakama ya Kadhi
Kuhusu uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi, taarifa
hiyo inasema, “Suala la uanzishwaji wa Mahakama hii nchini kama
tulivyotoa maoni yetu kwa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria (Januari
16, 2015); barua yetu kwa Waziri Mkuu na matamko mbalimbali yaliyokwisha
kutolewa kuhusu jambo hili; Mahakama ya Kadhi inakiuka misingi ya Taifa
hili kuwa na Serikali isiyokuwa na dini wala mfumo wa sheria unaobagua
raia wake kwa misingi ya dini.”
Chanzo: Mwananchi
Chanzo: Mwananchi
0 MAONI YAKO:
Post a Comment